HOMSO YA KABIDHIWA VIFAA KAZI VYA KUTOLEA MAFUNZO KWA NJIA MTANDAO

Posted on: June 10th, 2024

SERIKALI kupitia Wizara ya Afya imetoa vifaa kazi katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Songea kwa ajili ya kutolea mafunzo kwa njia ya mtandao (Tele-ECHO) ambayo yatawajengea uwezo wataalamu wa Afya katika utoaji huduma ya matibabu.

Akizungumza mara baada ya kukabidhiwa vifaa hivyo Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Songea Dr Magafu Majura amesema mfumo wa mafunzo kwa njia ya mtandao utasaidia kwa kiasi kikubwa kutoa mafunzo kwa watoa huduma za afya hususani maeneo ya vijijini.

Dr. Majura amesema mfumo huu utaweza kuwafikia watoa huduma huko waliko kwenye vituo vyao vya kazi kwani itarahisisha kuwafikia wengi kwa wakati mmoja.

"Naishukuru Serikali pamoja na shirika la afya ya Umma (CDC) kwa kuiwezesha Hospitali yetu kuwa kituo cha mafuzo haya ya mfumo wa Echo project, ambapo kupitia projecti hii tunategemea watumishi wa Afya waliopo Mkoa wa Ruvuma watapata mafunzo ambayo yatatolewa na watumishi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Songea" amesema Dr Majura.

Naye mratibu wa huduma za udhibiti UKIMWI Mkoa wa Ruvuma Dr. Josephat Kalipesa amesema mfumo huu wa mafunzo kwa njia ya mtandao umelenga katika utoaji elimu mbalimbali za afya hasa kwenye vituo vyote vya afya vilivyopo katika Halmshauri za Mkoa wa Ruvuma.

"Tunatoa shukrani kwa fursa hii kwani mafunzo kwa njia ya mtandao yatawezesha kufikisha elimu kwa urahisi ambapo mwanzo changamoto ilikuwa ufinyu wa bajeti ambapo ilibidi kuwakutanisha wataalamu sehemu moja ila kwa sasa itaepusha gharama (posho) za mikutano"amesema Dr Kalipesa